Pinda Awafariji Walioathirika na Ajali ya Mtubwi Kavuu Katavi

#msemajimkuuwaserikali #maelezotv #kaziiendelee
Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi na Mbunge wa Jimbo la Kavuu, katika halmashauri ya Mpimbwe mkoa wa Katavi, Mhe. Geophrey Pinda, amewatembelea na kuwafariji wananchi wa kijiji cha Ukingwamizi katika kitongoji cha Itumba kata ya Mwamapuri kufuatia watu saba kupoteza maisha kwa ajali ya Mtumbwi.
Ajali hiyo iliyotokea mwishoni mwa wiki kufuatia maji kutoka mto Kavuu kuzunguka maeneo ya kitongoji cha Itumba ambapo miili ya watu watano imeopolewa huku miili ya watu wawili ikiwa haijapatikana.
Akizungumza na wananchi wa kijiji Ukingwamizi tarehe 30 Mei 2024 mkoani Katavi, Mhe. Pinda amewapa pole wafiwa na kuwaeleza kuwa serikali iko pamoja nao katika kipindi hiki kigumu cha msiba wa ndugu zao waliopoteza maisha kwenye ajali.
‘’Serikali iko na nyie ndiyo maana mmeona walikuja na kulala hapa kuhakikisha wanafanikisha upatikanaji wa miili ya ndugu zetu’’ alisema Mhe. Pinda
Amewaambia wananchi wa kitongoji cha Itumba kuwa, baada ya ajali hiyo hivi sasa ni vyema wakaanza kuchukua tahadhari madhubuti kwa kuhakikisha vyombo vya usafiri wanavyotumia kwenye maji vinaimarishwa na kuangaliwa kila wakati kwa kuwa vikikaa muda mrefu vinaoza na hivyo kuwa rahisi kupitisha maji.

Пікірлер